Al-Quraysh ni sura ya 106 ya Qur'ani Tukufu ambayo ina aya 4 na iko katika Juzuu ya 30. Ni Makki na ni Sura ya 29 iliyoteremshwa kwa Mtukufu Mtume Muhammad (SAW).
Aya ya kwanza inaelekeza kwenye Kabila la Maquraishi na safari za majira ya kiangazi na kipupwe zilizochukuliwa na watu wake, na hivyo basi jina la sura hiyo.
Maquraishi lilikuwa moja ya makabila makuu na yanayojulikana sana huko Uarabuni na Mtukufu Mtume Muhammad (SAW) alikuwa mtu wa kabila hili.
Wafasiri wengi wa Qur'ani Tukufu wanaichukulia Sura Al-Quraysh kuwa ni mwendelezo wa Sura Al-Fil. Katika Sura Al-Fil, Quran inaelekeza kwenye vitisho vya maadui na majaribio yao ya kuiangamiza Ka'aba. Lakini katika Sura Al-Quraysh, inaangazia amani na utulivu ambao Kabila la Maquraish limeipata huko Makka, amani ambayo Muhammad (SAW) aliteuliwa kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu na kueneza Uislamu.
Aya ya pili katika Sura Al-Qurasyh inaelekeza kwenye safari za majira ya baridi na kiangazi za watu wa kabila hilo. Wangesafiri kwenda Yemen na Sham wakati wa kiangazi na kipupwe kwa ajili ya biashara. Safari hizi na shughuli za biashara ziliwasaidia kukuza hali bora za maisha na kuimarisha urafiki na umoja kati yao.
Baada ya Muhammad kuteuliwa kuwa Mtume (SAW), Maquraishi hawakuhitaji tena kusafiri kwa sababu watu kutoka pande zote za ardhi walikuwa wakija Makka kumuona Mtukufu Mtume (SAW) na huko pia waliuza bidhaa zao na watu wa Makka wangenunua chochote walichohitaji.
Ka’aba, pia, ilikuwa ni chanzo cha baraka kwa Waquraishi na Sura inasisitiza kwamba watu wa kabila wanapaswa kumwabudu Mola wa Nyumba ambaye aliwaokoa na njaa na ukosefu wa usalama.
"Basi wamuabudu Mola Mlezi wa Nyumba hii aliye walisha njaa na akawalinda na khofu." (Aya ya 3-4)