Sherehe hiyo iliandaliwa na wanafunzi wa Madani Jamia Masjid na Madrasah Tartil-ul-Qur'an, kwa msaada wa taasisi ya kidini ijulikanayo kama Rahmat Lal Alamin, jarida la The News International iliripoti Jumatano.
Wanazuoni na wanafunzi wa Kiislamu waliwakaribisha watoto wa Kikristo na baba zao kwa maua na salamu.
Mwenyekiti wa Rahmat Lal Alamin, Khurshid Ahmed Nadeem, alisema kuwa Waislamu na Wakristo wana mambo mengi yanayofanana.
Sherehe hiyo pia ilihudhuriwa na imamu wa msikiti huo na mwanazuoni maarufu wa dini, Maulana Syed Akbar Ali Shah, pamoja na viongozi wa Kikristo, kama vile Zakir Paul Advocate, Kasisi Peter Gill, Kasisi Paul Masih, Kasisi Cristofer, Kasisi Aslam Masih, na Mchungaji Nasir William. Mratibu wa hafla hiyo, Sabookh Syed, na wazungumzaji wengine pia walihutubia mkutano huo.
Wazungumzaji walisifu michango na dhabihu za watu wa dini zingine, wakiwemo Wakristo, kwa kuanzishwa na utulivu wa Pakistan, na kutaka kujumuishwa kwao katika mtaala.
Viongozi hao wa Kikristo walitoa shukrani na furaha kwa kualikwa kwenye sherehe hiyo ambayo walisema ni ya kwanza kufanyika nchini Pakistan.
Sherehe hiyo ilikuwa na visomo kutoka katika Qur'ani Tukufu na Biblia, na sherehe za kuzaliwa kwa Nabii Isa (amani iwe juu yake). Watoto hao pia walitoa hotuba ili kukuza maelewano kati ya Waislamu na Wakristo. Mwishoni, watoto wa Kiislamu walitoa chakula kwa watoto wa Kikristo na kuwapa mifuko ya shule na zawadi.
3486585