Ismail Hania amesisitiza kuwa, wananchi wa Palestina katu hawawezi kuridhia uvamizi wa Wazayuni katika ardhi za Palestina pamoja na ujenzi wa vitongoji haramu vya walowezi katika maeneo ya Wapalestina.
Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS amebainisha kuwa, umoja na mshikamano wa taifa la Palestina upo mstari wa mbele kwa ajili ya kukabiliana na adui mzayuni na kwamba, mapambano ndilo chaguo la kistratijia kwa ajili ya ukombozi wa Palestina.
Aidha Hania ameeleza kuwa, muqawama na mapambano ndio njia ya mkato kabisa kwa ajili ya kuwatimua wavamizi Wazayuni katika katika ardho za Palestina na kurejesha haki zilizoghusubiwa za Wapalestina na hivyo kuandaa uwanja wa kurejea katika ardhi zao za asili wakimbizi wa Kipalestina.
Hayo yanajiri katika hali ambayo, muqawama wa Palestina umesisitizia ulazima wa kuendelea kutoa mashinikizo kwa utawala haramu wa Kizayuni wa Israel na kueleza kwamba hautaruhusu wala kukubali mpango wa Kizayuni wa "Uchumi Mkabala wa Usalama". Katika siku za hivi karibuni utawala wa Kizayuni umekithirisha mauaji ya vijana wanamapambano Wapalestina.
Pamoja na hayo, hivi karibuni Israel ilipata pigo kubwa katika vita vya siku 12 vya 'Upanga wa Quds' huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu .
Vita hivyo vya siku 12 vilianzishwa na Israel dhidi ya Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi mwa Mto Jordan na Gaza kuanzia tarehe 10 Mei mwaka huu na kumalizika tarehe 21 mwezi huo huo baada ya utawala wa Kizayuni kuomba kusitisha mapigano baada ya kupokea kipigo kutoka kwa wanamapambano wa Palestina.