IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Moja ya njia ya kupunguza matatizo ya kijamii ni kuhimiza sala

18:56 - January 26, 2016
Habari ID: 3470091
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu moja ya njia yenye taathira kubwa katika kupunguza matatizo ya kijamii, ni kuhimiza sala.
Ayatullah Udhma Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameyasema hayo katika ujumbe kwa kikao cha ishirini na nne kikuu cha sala nchni Iran na huku akisisitizia udharura wa kila mmoja kuhisi kuwa ana jukumu la kueneza utamaduni wa kutekeleza vilivyo ibada ya Sala, amewataka watu wote na hususan maafisa wa taasisi husika na kila mwenye suhula za kimaada na kimaanawi na nafasi katika uongozi, kuelewa ukubwa na adhama ya suala hilo na kuchukua hatua za kivitendo kulifanikisha.
Matini kamili ya ujumbe wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ambao umesomwa leo (Jumanne) na Ayatullah Abedini, mwakilishi wa Kakihi Mtawala (Waliyyul Faqih) ambaye pia ni Imam wa Ijumaa wa mkoa wa Qazvin, katika kikao kikuu cha 24 cha Sala nchini Iran ni kama ifuatavyo:

Bismillahir Rahmanir Rahim
Ninamshukuru Mwenyezi Mungu Mweledi wa kila kitu na Mwenye nguvu, kwa jitihada zenu wahusika nyote wapendwa wa kusimamia na kuendesha kikao hicho muhimu, na zaidi kwa alimu mkubwa na mujahid, janab Hujjatul Islam Bw. Qaraati, jitihada ambazo zimezaa matunda mazuri katika sekta muhimu sana na zenye taathira kama ambavyo zimefanya kazi nzuri pia katika kueneza faradhi kubwa na isiyo na mbadala ya Sala.
Pamoja na hayo yote, nafasi na medani ya kazi na vile vile mahitaji na kiu ya jamii ya Kiislamu ya kufikia kwenye nukta inayotakiwa ni kubwa mno ikilinganishwa na mambo yaliyopo hivi sasa. Katika ujumbe wa mwaka jana, tulionesha sehemu fulani ya anga hiyo iliyo wazi na yenye nafasi ya kufanya juhudi za kujazwa nafasi hizo tupu.
Ujumbe wangu wa leo utasisitizia wajibu wa kila mtu kuhisi ana jukumu kubwa katika ufanikishaji wa jambo hilo. Mategemeo na matarajio yangu ni kuwa, watu wote na hususan maafisa wa taasisi husika na kila mwenye suhula za kimaada, kimaanawi na nafasi ya uongozi, wataelewa kwa njia sahihi adhama na ukubwa wa suala hilo na kuchukua hatua za kivitendo kulifanikisha.
Watu wote wanapaswa kuelewa kuwa, moja ya njia muhimu na zenye taathira kubwa katika juhudi za kupunguza matatizo na madhara katika jamii, ni kueneza utamaduni wa Sala. Litilieni hima suala la kueneza utamaduni huo na kuhakikisha unaenezwa kwa namna ambayo hakutakuwa na kijana wala barobaro yeyote nchini atakayedharau Sala. Hii ni moja ya njia bora kabisa za usalama wa kimaanawi na kiroho wa watu wetu na jamii yetu.
Vile vile lipeni umuhimu mkubwa suala la kuhakisha watu wote wanajifunza na kujizoesha kutekeleza ibada ya Sala kwa unyenyekevu mkuu na kuuhudhurisha moyo. Hayo yote ni mambo yanayowezekana kufanikishwa kwa azma ya kweli ya nyinyi wahusika wakuu na kwa kazi yenu ya kudumu na ya kuendelea katika suala hilo.
Wassalaamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakaatuh
Sayyid Ali Khamenei
Bahman 6, 1394
(Januari 26, 2016).

3470329

captcha