. Papa ambaye yuko ziarani barani Afrika amesema hayo mapema leo mjini Nairobi, Kenya alipokutana na viongozi wa kidini. Amesema kwamba ushirikiano miongoni mwa viongozi wa kidini ni njia moja ya wao kuelewa itikadi za wenzao na kuziheshimu. Viongozi wa Kiislamu wamemtaka Papa Francis kuingilia kati suala la wanafunzi wa Kiislamu wanaosomea shule za Kikatoliki kulazimishwa kushiriki kwenye shughuli za kanisa kama vile misa. Viongozi hao, kupitia mwenyekiti wa Baraza kuu la Waislamu Kenya, SUPKEM, Profesa Abdulghafur el Busaidi, wamesema kadhia hiyo inaleta mkwaruzano usiofaa kati ya Waislamu na Wakristo wa Kikatoliki.
Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani anatarajiwa kuelekea nchini Uganda hapo kesho kabla ya kumalizia safari yake ya nchi tatu za Afrika huko Jamhuri ya Afrika ya Kati mwishoni mwa wiki hii. Hii ni mara ya kwanza kwa kiongozi huyo wa kidini kuzuru Afrika tangu aliposhika hatamu za uongozi huko Vatican mwaka 2013.