IQNA

Hali ya Waislamu Uganda

Kamata kamata ya Waislamu nchini Uganda yaibua malalamiko

15:57 - December 06, 2022
Habari ID: 3476206
TEHRAN (IQNA)- Waislamu nchini Uganda kutoka makundi yote ya jamii jana Jumatatu walipinga kukamatwa kiholela kwa viongozi wa Waislamu wakati wa uvamizi wa misikiti.

Viongozi wa dini ya Kiislamu, wabunge, wafanyabiashara na wanajamii kwa pamoja walijitokeza kulaani utiaji mbaroni huo ambao wanaamini ni kinyume cha sheria na haustahili kufanywa.

Asuman Basalirwa, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wabunge Waislamu na ambaye anawakilisha eneo-bunge la Bugiri amesema: "Huu ni ubaguzi wa wazi wa serikali dhidi ya Waislamu. Mara kwa mara maafisa wa serikali wanavamia misikiti na kuwakamata kiholela masheikh bila ya kufuata sheria na kuwaweka mahabusu bila kuwafikisha mahakamani." 

Wabunge Waislamu wa Uganda pia wamelalamikia kuvunjiwa hserhiama Misikiti kunakofanywa na vyombo vya dola ambavyo maafisa wake huingia kwenye maeneo hayo matakatifu wakiwa wamevaa viatu.

Miongoni mwa waliokamatwa hivi karibuni ni naibu kiongozi wa madhehebu ya Tabligh Muslim nchini Uganda, Sheikh Yahaya Mwanje na Waislamu wengine zaidi ya 10. Wabunge hao Waislamu wametaka Sheikh Yahaya aachiliwe huru bila ya masharti yoyote na vyombo vya usalama viruhusu washukiwa wakutane na familia na mawakili wao au wafikishwe mahakamani ijulikane wamekamatwa kwa kosa gani.

Aidha wametaka Waislamu wengine wanaozuiliwa magerezani wafikishwe mahakamani na sheria ifuate mkondo wake kwa maafisa usalama wa serikali wanaovunja katiba kwa kuwakamata kiholela Waislamu hao. 

Mbunge wa Katikamu Kusini Hassan Kirumira amesema hawawezi kukaa kimya huku Waislamu wenzao wakitekwa nyara kinyume cha sheria.

Nalo Baraza Kuu la Waislamu wa Uganda limefanya mkutano na waandishi wa habari katika mji mkuu, Kampala, ambapo msemaji wa baraza hilo, Ashiraf Zziwa Muvawala, naye amelaani kukamatwa kiholela Waislamu hao.

Katika kipindi cha wiki nne zilizopita, vyombo vya usalama vya Uganda vimewatia mbaroni zaidi ya Waislamu 15 katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo.

Msemaji wa polisi, Fred Enanga amedai kuwa baadhi ya waliokamatwa wana kesi za kujibu na hivi karibuni watafikishwa mahakamani.

3481552

Kishikizo: uganda waislamu
captcha