IQNA

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran

Maendeleo ya kuridhisha katika mazungumzo ya Iran na Saudi Arabia

22:48 - September 24, 2021
Habari ID: 3474336
TEHRAN (IQNA)-Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa katika miezi michache iliyopita kumefanyika mawasiliano ya mara kwa mara kati ya Iran na Saudi Arabia na kuongeza kuwa, mazungumzo mazuri yamefanyika juu ya maswala yanayozihusu pande mbili.

Akizungumzia hali ya hivi karibuni ya mazungumzo ya Iran na Saudi Arabia, Saeed Khatibzadeh, amesema kuwa kumekuwepo mazungumzo kadhaa na serikali ya Saudi Arabia huko Baghdad katika miezi michache iliyopita na kuongeza kuwa, kuna maendeleo ya kuridhisha katika mazungumzo yanayohusiana na usalama wa Ghuba ya Uajemi.

Khatibzadeh amesisitiza kuwa, mazungumzo hayo hayajawahi kusimama na kwamba mawasiliano baina ya pande mbili yameendelea hata baada ya serikali mpya Iran kuanza kufanya kazi.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa, iwapo serikali ya Kifalme ya Saudi Arabia itatilia maanani ujumbe wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwamba suluhisho la matatizo ya eneo hili liko ndani ya eneo lenyewe na kwamba kuna ulazima kutafuta ufumbuzi wa kikanda, tunaweza kuwa na uhusiano endelevu na mzuri kati ya nchi mbili muhimu katika kanda hii ya Magharibi mwa Asia, yaani Iran na Saudi Arabia.

Katika hotuba yake kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Jumatano iliyopita, Mfalme Salman bin Abdulaziz Al Saud wa Saudi Arabia alielezea matumaini yake kuwa mazungumzo ya nchi yake na Iran yatajenga hali ya kuaminiana baina ya pande mbili.

84480999/

captcha