Katika taarifa yake, Dakta Najeeb Khalil al Qabati Msemaji wa Wizara ya Afya ya Yemen ametangaza kuwa, mashambulizi ya kila uchao ya muungano vamizi huko Yemen unaoongozwa na Saudi Arabia katika miaka kadhaa iliyopita yamesababisha kubomolewa kikamilifu vituo vya afya 527; huku asilimia 50 ya vituo hivyo vya huduma za afya vikishindwa kabisa kufanya kazi.
Wafanyakazi wa Wizara ya Afya ya Yemen jana Jumatatu walikusanyika mbele ya Ofisi ya Umoja wa Mataifa nchini humo kulalamikia kuendelea mashambulizi ya muungano vamizi wa Saudia na mzingiro dhidi ya Yemen pamoja na athari mbaya na hasara zilizosababishwa kwa sekta ya afya nchi hiyo.
Dakta Al Qabati ameongeza kuwa, wagonjwa 5,000 ambao wana matatizo ya figo wanahitajia kupandikizwa nyingine; lakini kufungwa uwanja wa ndege wa Sana'a kunatishia uhai wa wagonjwa hao.
Msemaji wa Wizara ya Afya ya Yemen ameeleza kuwa, kuzingirwa kwa pande zote nchi hiyo kumesabababisha kupatikana kwa nadra za matibabu ya magonjwa sugu; na asilimia 50 ya dawa muhimu za saratani hazipatikani.