IQNA

Afrika Kusini yaimarisha sekta ya utalii halali mjini Cape Town

20:56 - October 16, 2018
Habari ID: 3471710
TEHRAN (IQNA)- Meya wa mji wa Cape Town nchini Afrika Kusini Patricia de Lille amesema idadi Watalii Waislamu wanatarajiwa kuwa kati watakaoleta pato kubwa mjini humo.

Kufuatia ukweli huo mji wa Cape Town umetangaza azma ya kuimarisha sekta ya utalii halali ili kuwavutia watalii Waislamu wanaozingatia mafundisho ya Kiislamu.
De Lille ameyasema hayo Jumatatu katika ufunguzi wa Wiki ya Halal ya Afrika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano mjini Cape Town. Katika kikao hicho Bi. De Lille aliashiria nafasi muhimu ya utalii halali katika mji wa Cape Town na jimbo zima la Western Cape.
Wakuu wa sekta ya utalii wanapanga kuhakikisha watalii Waislamu wanapata huduma zote kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu.
Idadi kubwa ya watalii Waislamu Cape Town ni kutoka nchi kama vile Uturuki, Qatar, Umoja wa Falme za Kiarabu na Saudi Arabia.
Mapema mwaka huu Hoteli ya Hilton Cape Town ilitangaza kupanua huduma zake kuwavutia wasafiri Waislamu. Mbali na kuwapa wageni miswala na nakala za Qur'ani Tukufu wanapowasilisha ombi, vyumba pia vina alama za kuonyesha qibla. Halikadhalika vyoo vimejengwa kwa mujibu wa ustaarabu wa Waislamu.
Aidha mjini Cape Town kuna migahawa kadhaa inayomilikiwa na Waislamu ambayo inauza chakula halali kwa wasafiri. Halikadhalika mji huo una misikiti kadhaa huku msikiti mkubwa zaidi ukiwa Masjid Gatesville.
Utalii Halali ni istilahi inayotumika kumaanisha utalii unaolenga kuwavutia Waislamu na familia zao. Huu ni utalii ambao huzingatia kanuni na sheria za Kiislamu ambapo, kwa mfano hoteli husika huwa haziuzi pombe na wala majumba ya kamari n.k na wala wanawake na wanaume hawaogelei sehemu moja. Aidha hoteli kama hizo huhakikisha kuwa chakula kinachopikwa huwa ni halali na kwa mujibu wa mafundisho ya Kiislamu.

3466997

captcha